UWEZO WA AKILI YA BINADAMU NI WA AJABU NA USIOKADIRIKA! | JIFUNZE UJASIRIAMALI

UWEZO WA AKILI YA BINADAMU NI WA AJABU NA USIOKADIRIKA!



Kweli alikuwa ameingia katika Ulimwengu tofauti. Tulikuwa tumekataa kukubali kasoro za asili, na kwa shauku isiyokoma, tulikuwa tumeishawishi asili kurekebisha ile kasoro, kupitia njia pekee zinazowezekana zilizokuwepo.

Shauku ilikuwa imeanza kutupa gawio lakini ushindi ulikuwa bado haujakamilika. Kijana bado alitakiwa kutafuta njia muafaka na inayotekelezeka ya kubadilisha ulemavu wake kuwa rasilimali inayolingana nao.

Akiwa bado hajatambua vizuri umuhimu wa kile ambacho kilikuwa kimefanikishwa, lakini akiwa amechanganyikiwa kwa furaha ya ugunduzi wa Dunia yake mpya ya sauti, aliandika barua kwa watengenezaji wa kile kifaa cha kusaidia kusikia, akaelezea kwa shauku kubwa jinsi alivyojisikia. Kitu fulani kwenye barua yake- kitu fulani, pengine, ambacho hakikuandikwa kwenye mistari lakini kipo katikati yake- kiliifanya kampuni kumualika New York. Alipowasili, alitembezwa kiwandani.

Alipokuwa akizungumza na Injinia mkuu, akimuelezea juu ya dunia yake mpya, hisia, wazo, au mawazo ya kutia moyo- yaite vyovyote vile utakavyo, yalimulika katika akili yake. Ulikuwa ni huu msukumo wa mawazo uliobadilisha ulemavu wake kuwa rasilimali iliyokusudiwa kulipa gawio la pesa na furaha katika mamilioni kwa wakati wote ujao.

Wazo kuu la huo msukumo wa mawazo lilikuwa hili; lilimtokea ili kwamba aweze kuwa msaada kwa mamilioni ya watu wasiosikia ambao wameishi pasipo kupata fursa  ya kuwa na vifaa vinavyowawezesha kusikia, kama angeliweza kupata njia ya kuwaeleza habari za Ulimwengu wake mpya. Mara moja alifikia uamuzi wa kujitolea maisha yake yaliyobakia kutoa huduma zenye manufaa kwa watu wenye matatizo ya kusikia.

Kwa mwezi mzima alifanya utafiti wa kina. Alichanganua mfumo mzima wa soko la wazalishaji wa vifaa vya kusaidia kusikia, na kutengeneza njia na namna ya kuwasiliana na wenye matatizo ya kusikia Duniani kote kwa madhumuni ya kuwashirikisha Ulimwengu wake mpya aliougundua. Hili lilipofanyika, aliandika mpango wa miaka miwili akitumia matokeo ya utafiti alioufanya.

Katika kuwasilisha mpango kwenye kampuni, palepale alipewa cheo kwa lengo la kutekeleza mpango wake. Alipokwenda kufanya kazi hakuota kama alikuwa amekusudiwa kuleta matumaini na nafuu ya kweli kwa maelfu ya watu wasiosikia ambao pasipo msaada wake wangeliweza kuangamia milele kwenye uziwi-bubu.

Muda mfupi baada ya kuungana na watengenezaji wa kifaa chake cha kusikia, alinialika kuhudhuria darasa lililoendeshwa na kampuni yake kwa lengo la kuwafundisha wenye ulemavu wa kusikia na kusema ili waweze kusikia na kusema. Sikuwa nimewahi kusikia aina hii ya elimu kwa hiyo nilihudhuria darasa kwa tahadhari, lakini kwa matumaini kwamba muda wangu usingeweza kupotea bure.

Hapa niliona ufafanuzi ulionipa maono makubwa ya kile nilichokuwa nimekifanya kuamsha na kuweka hai katika akili ya kijana wangu shauku ya kuwa na usikivu wa kawaida. Nilishuhudia wenye ulemavu wa kusikia na kusema wakifunzwa kweli kusikia na kusema kupitia matumizi ya kanuni binafsi zilezile nilizokuwa nimetumia zaidi ya miaka 20 nyuma katika kumuokoa mwanangu kutokana na uziwi-bubu.

Hivyo kupitia mzunguko wa ajabu wa gurudumu la bahati, kijana wangu Blair na mimi tulijaliwa uwezo wa kurekebisha uziwi hata kwa wale ambao bado walikuwa hawajazaliwa. Hapana shaka akilini mwangu kuwa Blair angeliweza kuwa kiziwi maisha yake yote, ikiwa mimi na mama yake tusingelichukua hatua ya kutengeneza akili yake kama tulivyofanya.

Blair alipokuwa mtu mzima, Daktari Irving Voorhees, mtaalamu aliyebobea katika masuala hayo alimchunguza kwa makini. Alistaajabishwa pale alipogundua ni kwa kiasi gani mwanangu alikuwa anasikia na kusema vizuri, na  alisema uchunguzi wake ulionyesha kwamba “kinadharia, kijana asingeliweza kusikia  kabisa”. Lakini kijana alikuwa anasikia, licha ya ukweli kwamba picha za X-ray zilionyesha hakukuwa na uwazi katika fuvu lake, eneo ambalo masikio yake yalipaswa kuwa kuelekea kwenye ubongo.

Wakati nilipopandikiza katika akili yake shauku ya kusikia na kusema na kuishi kama mtu wa kawaida, msukumo huo uliambatana na nguvu isiyokuwa ya kawaida iliyosababisha Asili kugeuka kuwa kiunganishi na kuziba mwanya mkubwa wa ukimya kati ya ubongo wake na dunia ya nje kupitia njia fulani ambazo wataalamu wa afya waliobobea bado hawajaweza kuzitafsiri.

Ingeliweza kuwa ni kufuru kwa mimi hata kubashiri ikiwa ni jinsi gani Asili ilitenda huu muujiza. Ingelikuwa ni kitendo kisichosameheka kama ningelipuuzia kuuambia Ulimwengu kwa kadiri ninavyofahamu kuhusu sehemu japo ndogo ya huo uzoefu wa kushangaza. Ni wajibu wangu na fahari kusema ninaamini, na siyo pasipo sababu, kwamba hakuna linaloshindikana kwa mtu ambaye huipa nguvu Shauku kwa Imani stahamilifu.

Sina shaka kwamba shauku kuu ina njia zilizojificha za kujigeuza yenyewe kuwa kitu kinachoshikika kilichokuwa na ukubwa sawa nayo. Blair alitamani usikivu wa kawaida; sasa ameupata! Alizaliwa na ulemavu ambao ungeliweza kirahisi kumtuma mtu mwenye shauku kidogo barabarani akiwa na mzigo wa penseli na kikombe cha bati.

Ulemavu ule sasa unatarajia kuwa kiunganishi kitakachomsaidia kutoa huduma stahiki kwa mamilioni ya watu wenye matatizo ya kusikia, vilevile kumpatia ajira ya uhakika kwa ujira mzuri wa pesa katika maisha yake yote yaliyobakia.

Uwongo mweupe” kidogo niliopandikiza  ndani ya akili yake wakati alipokuwa mtoto mdogo na kumfanya aamini ulemavu wake ungeweza kugeuka na kuwa rasilimali kubwa ambayo angeweza kuitumia kama mtaji ulikuwa umehalalishwa. Hakuna chochote, kizuri au kibaya ambacho imani iliyochanganywa na Shauku kuu itashindwa kukigeuza kuwa kweli. Sifa hizi ni bure kwa kila mtu.

Katika uzoefu wangu wote wa kushughulika na wanaume na wanawake wenye matatizo binafsi, sikuwahi kushughulika na tatizo hata moja ambalo linaelezea dhahiri kabisa uwezo wa Shauku. Waandishi wakati mwingine hufanya makosa ya kuandika mada walizokuwa nazo lakini juujuu au kwa uelewa wa chini sana. Imekuwa bahati kwangu kuwa na upendeleo wa kufanya jaribio la utimilifu wa Uwezo wa Shauku kupitia ulemavu wa mtoto wangu mwenyewe.

Pengine ilikuwa ni bahati kwamba uzoefu ulikuja kama ulivyofanya, kwa kweli hakuna mwenye kujiandaa vyema kuliko vile atahudumu kama mfano wa kile kinachotokea wakati shauku inapofanyiwa majaribio. Ikiwa Mama Asili huinama kwa mapenzi ya Shauku, kuna mantiki kweli mtu wa kawaida tu aweze kuishinda Shauku kuu?

Uwezo wa akili ya binadamu ni wa ajabu na usiokadirika ! Hatufahamu njia ambayo hutumia kila hali, kila mtu, kila kitu kinachoweza kushikika kilichokuwa ndani ya uwezo wake kama njia za kugeuza shauku kuwa kitu halisi chenye ukubwa unaolingana nayo. Labda sayansi itagundua siri hii. Nilipandikiza akilini mwa kijana wangu shauku ya kusikia na kusema kama mtu yeyote yule wa kawaida anavyosikia na kusema.

Shauku ile sasa imegeuka kuwa kweli. Nilipandikiza akilini mwake shauku ya kubadilisha ulemavu wake mkubwa kabisa kuwa rasilimali yake kubwa kabisa. Shauku hiyo imeshuhudiwa. Mbinu zilizotumika kuleta matokeo haya ya kushangaza siyo vigumu kuzielezea. Zina vitu vitatu vyenye ukweli kamilifu. Cha kwanza, NILICHANGANYA IMANI na SHAUKU kwa ajili ya usikivu wa kawaida, ambavyo nilivihamishia kwa mwanangu.

Pili, niliwasilisha shauku yangu kwake katika kila njia inayowezekana iliyokuwepo kupitia uvumilu, juhudi endelevu, kwa kipindi cha miaka mingi. Tatu, ALINIAMINI MIMI.

Miaka kadhaa nyuma, mmoja kati ya washirika wangu kibiashara alikuwa mgonjwa, hali yake iliendelea kuwa mbaya kadiri muda ulivyokuwa ukipita, na mwishowe alipelekwa hospitalini kwa ajili ya upasuaji. Punde tu kabla hajapakizwa kwenye baiskeli ya magurudunu matatu kuelekea chumba cha upasuaji nilimuangalia na kushangaa ni kwa jinsi gani mtu mwembamba na aliyedhoofu  kiasi kile angeliweza kufanyiwa upasuaji mkubwa na akatoka salama.

Daktari alinionya kwamba, kulikuwa na uwezekano mdogo sana, kama upo wa mimi kuja kumuona tena akiwa hai. Lakini hayo yalikuwa ni maoni ya Daktari.  Hayakuwa maoni ya mgonjwa mwenyewe. Punde kabla hajapelekwa, alininongoneza kwa unyonge; “Usiwe na wasiwasi bosi wangu, nitatoka hapa siku siyo nyingi”.

Muuguzi aliyekuwa akimwangalia alinitazama kwa huzuni. Lakini mgonjwa alikuja kutoka salama !  Baada ya kila kitu kwisha, daktari wake alisema; “Hakuna kitu kingine zaidi ya shauku yake ya kuishi kilichoyaokoa maisha yake. Kamwe asingeweza kutoka, ikiwa asingekataa kukubali uwezekano wa kifo”.

Ninaamini katika nguvu ya Shauku ikisaidiwa na Imani  kwa sababu nimeona hii nguvu ikiwainua watu kutoka mwanzo duni mpaka ngazi ya madaraka na utajiri; nimeiona ikipora makaburi ya wahanga wake; nimeiona ikihudumu kama jukwaa ambalo watu hulitumia kurudi baada ya kuwa wamefeli mara tofauti 100. Nimeiona ikimpatia kijana wangu mwenyewe furaha ya kawaida, maisha yenye mafanikio, licha ya Asili kumtuma Duniani bila ya kuwa na masikio.

Ni kwa jinsi gani mtu anaweza akaitumia nguvu ya Shauku?. Hili limekuwa likijibiwa kupitia sura hii, na sura zinazofuata za kitabu hiki.

Natamani kufikisha wazo kwamba mafanikio yote, bila kujali asili yake ikoje wala lengo lake, ni lazima yaanze na Shauku kubwa ya kukipata kitu halisi. Kwa kupitia kanuni fulani za ajabu na zilizokuwa na nguvu ndani ya “kemia ya akili”, asili huficha ndani ya msukumo wa shauku kuu ‘kitu hicho fulani’ ambacho hakitambui kamwe neno, ‘haiwezekani’ wala kukubali ukweli kama kufeli.
........................................................................................................


*Ndugu msomaji wetu na hii ndiyo sehemu ya mwisho (ya7 ) ya Sura hii ya pili, karibu uendelee kusoma sura ya Tatu........






0 Response to "UWEZO WA AKILI YA BINADAMU NI WA AJABU NA USIOKADIRIKA!"

Post a Comment