MUNGU HUTENDA KWA NAMNA YA AJABU ! | JIFUNZE UJASIRIAMALI

MUNGU HUTENDA KWA NAMNA YA AJABU !

Kwa kiasi fulani ningeliweza kutafuta njia ya kupandikiza ndani ya akili ya mtoto shauku yangu kuu ya kupata njia na namna ya kufikisha sauti kwenye ubongo wake bila ya kutumia masikio.

Pindi tu mtoto angefikisha umri wa kutambua, ningeliweza kuijaza akili yake kikamilifu kwa shauku kuu ya kusikia kiasi kwamba asili kwa kutumia njia zake yenyewe ingeweza kuitafsiri kuwa ukweli wenye kuonekana. Fikra zote hizi zilitokea ndani ya akili yangu mwenyewe, na sikumwambia mtu yeyote. Kila siku nilirudia tena upya ahadi niliyokuwa nimejiwekea mwenyewe ya kutokukubali ububu-kiziwi kwa kijana wangu.

Kwa kadiri alivyokuwa akikua na kuanza kutambua mazingira yaliyomzunguka , tuligundua kuwa alikuwa na uwezo kidogo wa kusikia. Alipofikisha umri ambao kwa kawaida watoto huanza kuzungumza, hakuonesha dalili za kuzungumza, lakini tuliweza kutambua kupitia vitendo vyake kwamba aliweza kusikia baadhi ya sauti kidogo. Hicho ndicho nilichokuwa nataka  kufahamu! Nilishawishika kwamba, ikiwa aliweza kusika, hata kama ni kwa kiasi kidogo angeliweza bado kuongeza uwezo mkubwa zaidi wa kusikia.

Halafu, kitu fulani kilitokea ambacho kilinipa matumaini. Kilitoka kwa chanzo ambacho hakikutegemewa kabisa- tulinunua record player, mtoto aliposikia muziki kwa mara ya kwanza, alijawa na furaha ya ajabu, na mara moja aliikubali ile mashine. Haraka alionyesha mapenzi kwa baadhi ya rekodi, miongoni mwao ni, ‘It’s a long way to Tipperary’. Katika tukio moja, alikicheza kibao hicho tena na tena kwa karibu saa mbili, akiwa amesimama mbele ya record player huku meno yake akiwa ameyakita ukingoni mwa kasha la player.

Umuhimu wa tabia hii aliyojijengea mwenyewe haukujidhihirisha wazi kwetu mpaka miaka ya baadaye kwani kwa wakati ule hatukuwa tumewahi kusikia kanuni ya “Sauti kusafiri kupitia mfupa(bone conductivity of sound).

Muda mfupi baada ya kuwa ameikubali ile record player, niligundua kwamba aliweza kunisikia vyema nilipozungumza midomo yangu ikiwa imegusa mfupa wake nyuma ya sikio, au kichwani chini ya ubongo.

Ugunduzi huu ulinifanya niwe na nyenzo muhimu ambazo kwa kupitia hizo nilianza kutafsiri kuwa kweli Shauku yangu kuu ya kumsaidia kijana wangu kutengeneza uwezo wa kusikia na kusema.

Kipindi hicho alikuwa akijaribu kwa shida kusema baadhi ya maneno. Mwelekeo haukuwa unaridhisha lakini shauku ikisaidiwa na imani haijui neno liitwalo “haiwezekani”

Baada ya kujiridhisha kwamba alikuwa anaweza kusikia sauti yangu vizuri, nilianza mara moja kuhamishia kwenye akili yake shauku ya kusikia na kusema. Haraka niligundua kwamba mtoto alikuwa akifurahia hadithi wakati wa usiku, hivyo nilianza kazi ya kutunga hadithi zenye kumjengea hali ya kujitegemea, ubunifu na hamu kubwa ya kusikia na kuwa katika hali ya kawaida.

Kulikuwa na hadithi moja mahsusi ambayo niliiwekea msisitizo kwa kuipamba kwa nakshi mpya kila wakati iliposimuliwa. Ilitengenezwa kupandikiza kwenye akili yake mawazo kwamba hali yake ya ulemavu haikuwa ni mkosi bali ilikuwa ni rasilimali yenye thamani kubwa.

Licha ya ukweli kwamba falsafa zote nilizokuwa nimezichunguza vyema zilionyesha kwamba  kila mkosi huja  ukiwa ndani yake  umebeba mbegu ya neema inayolingana na mkosi wenyewe, ni lazima nikiri kwamba  sikuwa na wazo hata kidogo la jinsi ambavyo huu ulemavu ungeweza kubadilika  kuwa rasilimali.

Hata hivyo niliendelea na kitendo cha kuifungasha  hiyo falsafa ndani ya hadithi za usiku nikitumaini kuwa  muda ungeweza kufika ambapo angeweza kupata njia ambayo ulemavu wake ungeliweza kubadilishwa ukaweza kutumika kwa malengo yenye manufaa.

Mantiki iliniambia wazi kuwa kulikuwa hakuna mbadala wa kutosha wa upungufu wa uwezo wa asili wa kusikia. Lakini Shauku ikisaidiwa na Imani iliisukuma mantiki pembeni, na kunitia moyo kuendelea mbele.

Nikichanganua uzoefu huo kwa kufikiria ya nyuma, naweza kuona sasa kwamba imani ya kijana wangu kwangu ilikuwa na dhima kubwa kwa matokeo hayo ya kushangaza. Hakuhoji chochote kile nilichomwambia. Nilimuuzia wazo kwamba alikuwa na fursa ya kipekee kumshinda kaka yake, na hivyo fursa hiyo ingeweza kujiakisi yenyewe kwa namna nyingi.

Kwa mfano waalimu shuleni wangeweza kuona kuwa alikuwa hana masikio, na kwa sababu hiyo, wangeliweza kumpa uangalizi wa kipekee na kumtendea wema usiokuwa wa kawaida. Walifanya hivyo mara zote. Mama yake alilihakikisha hilo kwa kuwatembelea walimu na kupanga nao kumpa mtoto uangalizi wa ziada uliohitajika.

Nilimuuzia wazo pia kwamba wakati atakapokuwa na umri wa kutosha kuuza magazeti (kaka yake alikuwa tayari ameshaanza kuuza magazeti) angeweza kuwa na fursa ya kipekee kumshinda kaka yake kwani watu wangeliweza kumlipa pesa  za ziada  kwa huduma zake kwa sababu wangeweza kuona alikuwa ni mwenye akili, kijana mchapakazi, licha ya sababu kwamba alikuwa hana masikio.

Tuligundua kwamba, taratibu uwezo wa mtoto kusikia ulikuwa ukiongezeka. Zaidi ya hapo, hakuwa na kawaida yeyote ya kujitambua binafsi juu ya ulemavu wake. Alipofikisha miaka saba alionyesha ushahidi wa kwanza kuwa njia yetu ya kuboresha akili yake ilikuwa inazaa matunda.

Kwa kipindi cha miezi kadhaa alikuwa akiomba apewe ruksa ya kuuza magazeti, lakini mama yake asingeweza kumpa ruksa, alikuwa anaogopa kwamba uziwi wake ungesababisha hatari kwa yeye kuingia barabarani mwenyewe. Mwishowe jambo hili aliamua alifanye peke yake. Mchana mmoja alipoachwa nyumbani na mfanyakazi, alipanda kupitia dirisha la jiko, akarukia chini na kuanza kivyake.

Alikopa senti sita za mtaji kutoka kwa jirani yao aliyekuwa fundi viatu, alipata faida senti 42. Tulipofika nyumbani usiku ule, tulimkuta kitandani akiwa amelala huku mkononi akiwa ameshikilia kwa nguvu zile pesa. Mama yake aliufungua ule mkono wake, akaondoa sarafu na kisha kulia.

Katika yote, kulia juu ya ushindi wa kwanza wa mwanawe, ilionekana siyo sahihi. Mrejesho wangu ulikuwa kinyume. Nilicheka sana, kwani nilijua kwamba juhudi zangu kupandikiza ndani ya akili ya mtoto mtazamo wa kujiamini zilikuwa zimefanikiwa. Mama yake alichokiona katika ujasiriamali wake huu wa mwanzo ni; mvulana mdogo kiziwi ambaye alikuwa ameingia barabarani na kuhatarisha maisha yake ili kupata pesa.

Nilichokiona ni; mfanyabiashara mdogo jasiri, mwenye nia, mwenye kujitegemea ambaye uwezo ndani yake ulikuwa umeongezeka kwa asilimia 100 kwa kuwa alikuwa ameingia kwenye biashara akitumia uwezo wake mwenyewe, na alikuwa amefanikiwa. Mwamala uliniridhisha kwa sababu nilijua alikuwa ametoa ushahidi wa sifa ya uwerevu ambayo ingeweza kumkaa maisha yake yote. Matukio ya baadaye yalikuja kuthibitisha hili kuwa kweli.

Kaka yake alipotaka kitu fulani angeweza kugharaghara chini, kurusharusha miguu yake hewani akilia  mpaka akipate. Wakati “mvulana mdogo kiziwi” alipotaka kitu, angeweza kupanga jinsi ya kupata pesa, na kisha kujinunulia mwenyewe. Bado anaendelea kufuata njia hiyo!

Ukweli, kijana wangu mwenyewe amenifunza ya kuwa ulemavu unaweza ukageuzwa kuwa mawe ya kuvukia , ambayo mtu anaweza akayatumia kupanda kufikia malengo yenye thamani ikiwa hautapokewa kama kikwazo na kutumiwa kama kisingizio.

Mvulana mdogo kiziwi alipita madarasa, sekondari na chuo pasipo kuweza kuwasikia walimu wake, isipokuwa pale walipopaza sauti kwa nguvu, wakiwa karibu. Hakwenda shule ya viziwi. Tusingeliweza kumruhusu kujifunza lugha ya ishara. Tulidhania kwamba, alipaswa kuishi maisha ya kawaida na kushirikiana na watoto wa kawaida, na tuliusimamia uamuzi huo, ingawa ulitugharimu mijadala mingi mikali na maafisa wa shule.

Kipindi alipokuwa sekondari, alijaribu vifaa vya kusikia vya umeme, lakini havikuwa na manufaa yeyote kwake. Tuliamini hii ilitokana na hali iliyogundulika wakati mtoto alipokuwa na umri wa miaka sita. Daktari J. Gordon Wilson wa Chicago alimfanyia mtoto upasuaji katika upande mmoja wa kichwa chake na kugundua kwamba hakukuwa na dalili ya viungo vya asili vya kusikia.

Katika juma lake la mwisho chuoni (miaka 18 baada ya upasuaji) kitu fulani kilitokea ambacho kiliweka alama katika hatua muhimu zaidi ya maisha yake. Kupitia kile kilichoonekana kutokea kwa bahati, alikuja kuwa na kifaa kingine cha umeme cha kusikia ambacho alitumiwa kwa ajili ya majaribio.

Alikuwa mzito katika kukijaribu kutokana na kuvunjwa moyo na kifaa kingine kama hicho. Mwishowe aliinua kile kifaa kama vile hataki na kukiweka kichwani, akafunga betri, na lo!  kama vile kwa pigo la mazingaombe, HAMU YAKE YA MUDA MREFU YA KUSIKIA KAWAIDA ILIKUWA IMEGEUKA KUWA KWELI!  Kwa mara ya kwanza katika maisha yake alisikia kama mtu mwingine yeyote  yule mwenye usikivu wa kawaida.

“Mungu hutenda kwa namna ya ajabu”. Akiwa na furaha iliyopindukia kutokana na Ulimwengu tofauti ulioletwa kwake kupitia kifaa chake cha kusikia, alikimbia kwenye simu akampigia mama yake, na kusikia sauti yake vizuri. Siku iliyofuata aliisikia barabara sauti ya profesa wake darasani kwa mara ya kwanza katika maisha yake! Alisikiliza redio. Alisikiliza sinema. Kwa mara ya kwanza katika maisha yake, aliweza kuwasiliana kwa uhuru na watu wengine pasipo wao kupaza sauti.

.....................................................................................................

0 Response to "MUNGU HUTENDA KWA NAMNA YA AJABU !"

Post a Comment